Mohamed
Said
Mzee
Yusuf Halimoja karudi tena safari hii anasema katika kichwa cha makala yake,
“Sijasema Uhuru Uliletwa na Nyerere” (Jamhuri Januari 31 Februari 6 2012).
Katika makala hii wakati mnakasha (majadilano)unanoga yeye katangaza kuwa
anajitoa. Waswahili tuna msemo, “ametoa mbukwa.” Juu ya huko kujitoa madam
kanitaja katika makala yake sina budi nami kumpa majibu yangu katika yale
niyajuayo katika historia ya uhuru wa Tanganyika. Mzee Halimoja labda kwa utu
uzima huwa anasema mengi. Mimi sitajibu kila aliloandika ila nitapita mle
ambamo nahisi wasomaji watafaidika na kitu kipya ambacho hawakuwa wakikijua
kabla ya hapo.
Si
kweli kuwa Nyerere aliongoza juhudi za uhuru peke yake. Nyerere kaja Dar es
Salaam mwaka 1952 na akapokelewa na rais wa TAA Abdulwahid Sykes na alikuta
mambo yako mbali sana. Kirilo kenda UNO na kurudi, TAA ishazungumza
na Kamati ya Umoja wa Mataifa inayosimamia nchi zilizokuwa chini ya Udhamini na
ishapeleka mapendekezo ya katiba kwa Gavana Twining, TAA imeshaunda Kamati ya
Siasa na ikapeleka viongozi wake (Abbas Sykes, Japhet Kirilo na Saadan Abdu
Kandoro) kutembea nchi nzima kuzungumza na wananchi kuhusu madhila
ya ukoloni. Juu ya hayo yote TAA imeshafanya uhusiano na vyama
vingine vya siasa kama African National Congress (ANC) ya Northern Rhodesia
chini ya Kenneth Kaunda. (Ally Sykes hadi leo ana barua kadhaa alizokuwa
akiandikiana na Kaunda kabla Kaunda hata hajauana na Nyerere). Vilevile
Abdulwahid alikuwa kafanya mkutano na Kenyatta wakati wala Kenyatta hajasikia
jina la Nyerere. Nia ya mikutano hii ilikuwa kuunganisha juhudi za TAA na KAU
katika kupambana na Waingereza.
Kwa
wengi mambo haya ni mageni katika masikio yao wameleweshwa na propaganda za TAA
hakikuwa chama cha siasa. Simlaumu Mzee Halimoja naamini kabisa kuwa yeye haya
hakuwa anayajua. Kwa Mzee Halimoja siasa Tanganyika haikuwezekana bila Nyerere
na TANU chama ambacho Nyerere mwenyewe wala hana chimbuko nacho. Halimoja
anazungumza kuhusu ujasiri wa Nyerere. Sawa hapana neno lakini je anaujua
ujasiri wa Schneider Abdillahi Plantan katika TAA kiasi ambacho Waingereza
walimkamata na kumweka kuzuizini? Je Halimoja anajua kisa cha Dome Okochi
Budohi Mkenya kadi yake ya TANU na 6 kazi aliyokuwa akifanya katika harakati za
TAA kabla hawajaunda TANU akiwa ndiye kiunganisho kati ya TAA na KAU ya
Kenyatta? Ninaweza kumpa mifano kocho. Budohi alikamatwa mwaka 1955 pamoja na
wanaharakati wengine wa Kenya kwa tuhuma za kuwa Mau Mau. Budohi alifungwa
kisiwa cha Lamu kuazia 1955 hadi 1963 Kenya ilipokuwa inakaribia kupata uhuru
ndipo alipoachiwa. Budohi akifahamiana vyema kabisa na wazee wangu na
nimejifunza mengi kutoka kwake kuhusu TAA na TANU. Lakini kama Mzee Halimoja
anataka kubaki na historia ya Nyerere inayoanza na TANU 1954 na kupuuza
michango ya wengine mimi sina ugomvi na hilo. Naamini kwa haya machache msomaji
kapata yale ambayo hakuwa anayajua kabla na keshatambua kuwa TAA kilikuwa chama
cha siasa hata kabla Nyerere hajakutana na Abdu Sykes Dar es Salaam mwaka 1952.
Mzee
Halimoja kazungumzia kuhusu Abdulwahid Sykes kuwa kwa nini natumia rejea zake.
Napenda kumafahamisha kitu kimoja. Historia ya Nyerere na TANU itakuwa salama
na ikafahamika kama inavyofahamika katika historia rasmi mfano wa hii ya Mzee
Halimoja ikiwa tu Abdulwahid Sykes utamtoa katika historia ya TAA na TANU na
historia ya Nyerere mwenyewe. Lakini pale tu utamkapomleta marehemu Abdu katika
historia ya TAA na TANU itakubidi uachane na Nyerere kwanza na urudi robo karne
nyuma kupata mwanzo wa harakati na hapo ndipo unapambana na Nyaraka za Sykes na
hazitakuwa za Abdulwahid bali za baba yake. Hapo ndipo utakapojua umuhimu wa
nyaraka hizi. Kueleza yaliyomo humo katika nyaraka hizo inataka mada
itakayojitegemea yenyewe kwani ni historia inayorudi nyuma karne moja. John
Iliffe aliondoka na baadhi ya nyaraka hizi ambazo alikabidhiwa na binti yake
Abdu Sykes, Daisy Aisha wakati Daisy alipokuwa mwanafunzi wake wa historia
miaka ya 1960 katikati Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam na Iliffe hajazirejesha
hadi leo. Nyaraka hizo ndizo zilizomsaidia Illife kuandika historia ya TAA. Kwa
nini historia ya harakati ipatikane kwa mtu mmoja tu Abdu Sykes kama
anavyouliza Mzee Halimoja, jibu lake ni hili, baba yake Abdu Kleist Sykes ndiye
aliyeasisi harakati za siasa Tanganyika mwaka 1929 na ameacha nyuma hazina
kubwa ya maandiko. Anaetaka kujua zaidi na asome “Kleist Sykes, The Townsman”
na Daisy Sykes katika “Modern Tanzania,” kitabu kilichohaririwa na John Illife.
Mzee
Halimoja anasema Nyerere ndiye aliyeandika katiba ya TANU. Nataka nimweke sawa
Mzee Halimoja kuhusu katiba ya TANU. Katiba ya TANU haikuandikwa na yeyote
yule. Kwa ufupi ni kuwa Nyerere hakuandika katiba ya TANU. TAA Political Sub
Committee ilinakili katiba ya Convention Peoples Party (CPP) ya Kwame Nkrumah
neno kwa neno. Mzee Halimoja akitaka ushahidi aitafute katiba ya CPP na
aifananishe na katiba ya TANU. Hilo la kwanza. Kitu cha pili napenda
kumsahihisha kwa heshima zote Mzee Halimoja kuwa hiyo ilani namba 14 aliyoeleza
kuwa ilitolewa na Waingereza haikuwa namba 14 bali namba tano ikijulikana kama
Government Circular No. 5 (1 August 1953) ikiwakumbusha viongozi wa TAA
kutojiingiza katika siasa. Haya yalitokea baada ya serikali kuwa na ushahidi
kuwa TAA ilikuwa inafanya siasa dhahir shahir jambo ambalo Mzee Halimoja hataki
kulisikia sharti siasa iwe na Nyerere yumo. Baada ya kuona akina Abdu Sykes na
Hamza Mwapachu hawasikii wameshikilia tu kuwasakama Waingereza na serikali yao
ikatoka Government Circular No.6. Hapa kuna kisa cha kuhadithia lakini kwa
makala hii tutajitoa nje ya maudhui. Kipindi hiki wengi walikikimbia chama
wakabaki wanamji. Abdulwahid ilibaki kidogo apoteze kazi yake kama Market
Master Soko la Kariakoo. Hii ndiyo historia ya siasa ya TAA na TANU niijuayo
mie, historia ambayo wazee wangu walikuwa wachezaji wa kikosi cha kwanza na
wakinihadithia siku zote hadi walipotangulia mbele ya haki. Jambo la tatu Mzee
Halimoja hasemi kweli kuhusu historia ya TANU katika sehemu zile ambazo kanisa
lilikuwa na nguvu. Ukweli ni kuwa waliochelewa kuingia TANU si Warufiji na
Wangindo bali watu wa Masasi, Peramiho na kwengineko kutokana na shinikizo la
Kanisa. Niruhusu msomaji mpenzi nikudokolee kidogo mambo kutoka katika hazina
ya wazee wangu.
Mkutano
wa kwanza wa TANU 1955 ulihudhuriwa na Salum Mpunga na Ali Ibrahim Mnjawale
kutoka Lindi. Mkutano huu ulifanyika Dar es Salaam Ukumbi wa Hindu Mandal.
Baada ya mkutano, wakati wajumbe wengine wanaondoka kurudi kwenye majimbo
yao, Mpunga na Mnjawale walibakia nyuma kukutana na uongozi wa makao makuu wa
Julius Nyerere, Sheikh Suleiman Takadir, John Rupia, Ali Mwinyi Tambwe, Said
Chamwenyewe, Oscar Kambona na wengineo. Mpunga na Mnjawale waliwafahamisha
viongozi wa makao makuu kuhusu hali mbaya ya siasa Jimbo la Kusini. Mbali na
kampeni za kuipinga TANU za Liwali Yustino Mponda ambae Mzee Halimoja
anamfahamu vyema kabisa, katika ziara yake Lindi Gavana Twining
aliwatahadharisha Waafriika wa Tanganyika wasijihusishe na “wafanya fujo”
wanaotaka kuzusha vurugu. Twining alikuwa akitoa onyo hili akiikusudia TANU.
Hotuba hii ya Gavana iliwatisha wananchi wengi kutoka sehemu za kusini kujiunga
na TANU.
Mpunga
na Mnjawale waliomba Nyerere aende majimbo ya kusini kuhamasisha wananchi ili
wakabiliane na fitna za Gavana Twining na kampeni za kupinga TANU zilizokuwa
zikiendeshwa na Liwali Yustino Mponda. Ukweli ni kuwa Nyerere hakutaka kwenda
katika ziara ile akijua kuwa huko alikuwa anakwenda kupambana na kanisa lake
uso kwa macho. Juu hayo yote Mpunga na Mnjawale katika kikao kile
walimsisitizia Nyerere umuhimu wa yeye kwenda Lindi ambako kunaweza kuwa ndiyo
chanzo cha TANU kupata ufanisi Newala, Songea, Tunduru na Masasi ambako
kulikuwa na upinzani mkubwa dhidi ya TANU. Katika sehemu hizo Kanisa lilikuwa likiwazuia
Wakristo kujiunga na TANU. Sheikh Suleiman Takadir, Said Chamwenye, John Rupia,
Ali Mwinyi Tambwe wote waliunga mkono ule ujumbe wa Lindi juu ya suala hili.
Baada ya kufikia makubaliano, Mpunga na Mnjawale walipewa barua ya kuthibitisha
safari ya Nyerere. Ali Mwinyi Tambwe na Rajab Diwani walifuatana na Nyerere
kwenda Jimbo la Kusini kuondoa wasiwasi na woga uliozushwa na Gavana Twining na
kibaraka Yustino Mponda.
Nyerere
na msafara wake ulipokelewa na uongozi wa TANU wa Lindi huko Mbanji, kijiji
kidogo nje ya mji. Msafara wa Nyerere ulipowasili Mbanji ilikuwa kiasi cha saa
moja jioni hivi na giza lilikuwa linaanza kutanda. Mbali na Mpunga na wale
wajumbe wawili waliokutana na Nyerere mjini Dar es Salaam mwezi uliopita,
hakuna hata mtu kati ya umma ule uliokuja kupokea ujumbe kutoka makao makuu ya
TANU aliyekuwa anajua Nyerere anafanana vipi. Mpunga, dereva wa lori,
alijibagua kutoka kwa lile kundi la watu akawa amesimama pembeni ili Nyerere
apate kumuona. Baada ya Nyerere kumtia Mpunga machoni, Mpunga alimwendea
kumsalimu Nyerere, Tambwe na Diwani; kisha aliligeukia lile kundi la watu
kumtambulisha Nyerere kwa wananchi akilitaja jina lake kwa sauti kubwa. Baada
ya hapo aliutambulisha ule ujumbe wa Nyerere. Nyerere na ujumbe wake
ulisindikizwa kwa shangwe na kundi la watu hadi ofisi ya TANU kwenye nyumba ya
Suleiman Masudi Mnonji. Kupakana na ofisi ya TANU ilikuwepo nyumba ya seremala
mmoja, Issa bin Ali Naliwanda. Hii ndiyo nyumba iliyochaguliwa alale Nyerere na
ujumbe wake, si kwa sababu ilikuwa nzuri kupita zote. Ilichaguliwa na kupewa
heshima hii kwa sababu ilikuwa karibu sana na ofisi ya TANU na hivyo basi
ilirahisishia TANU kazi ya ulinzi wa Nyerere. Siku iliyofuata ilikuwa Jumapili
na Nyerere aliwaomba wenyeji wake apelekwe kanisani kwa ajili ya ibada.
Kanisa
Katoliki mjini Lindi ni jengo la fahari lililoko ufukweni katika Bahari ya
Hindi. Lindi ulikuwa mji wa Waislam. Mbali na mlio wa kengele za kanisa hakuna
mtu pale mjini aliyekuwa akishughulishwa na kile kilichokuwa kikifanyika kwenye
viwanja vya kanisa. Watu wachache waliokuwa wakienda kusali kanisani walikuwa
Wakristo waliokuja Lindi kutoka sehemu nyingine za Tanganyika kufanya kazi
katika ofisi za serikali. Ghafla mahala hapa palipokuwa pweke, palipopuuzwa kwa
miaka na Waislam wa mjini, pakawa muhimu kwa sababu rais wa TANU ambae alikuwa
Mkatoliki alikuwa na haja ya kuhudhuria ibada pale kanisani. Hakuna mtu katika
uongozi wa TANU wa Lindi aliyejua ndani ya kanisa lile kulikuwa vipi wala
hapakuwa na yoyote kati yao aliyewahi kuingia ndani ya kanisa, si Lindi wala
mahali popote pale. Uongozi wa TANU wa Waislam mjini Lindi haukumwamini Mkristo
yoyote kumsindikiza Nyerere kanisani ili kumpa ulinzi. Baada ya kujadili suala
hilo kwa urefu hatimaye iliamuliwa kuwa Mpunga na wanachama wachache Waislam
wenye kuaminika lazima wamsindikize Nyerere kanisani na wengine wabakie nje
kulinda mlango.
Jumapili
hiyo Nyerere aliingia ndani ya kanisa Katoliki mjini Lindi akifuatwa nyuma na
walinzi wake Waislam wakiongozwa na Salum Mpunga, dereva wa lori shupavu. Misa
hii maalum ilidumu katika fikra za wale Wakristo waliokuwepo pale
kanisani kwa miaka mingi kwa kuwa tukio hilo liliwagusa sana Wakristo
walioshuhudia mkasa ule ndani ya kanisa la Lindi. Hii huenda ilikuwa mara ya
kwanza na ya mwisho kwa Nyerere kumsalia Mungu wake huku akiwa amesimamiwa na
Waislam. DC mkoloni alikataa kutoa kibali kwa TANU kufanya mkutano wa hadhara.
Akiwa amekasirika sana, Shabaan Msangi aliitisha mkutano wa dharura wa tawi
uliohudhuriwa na Nyerere na Tambwe. Baada ya mkutano huo Tambwe alikwenda
kumwona DC. Ruhusa ilitolewa, na adhuhuri hiyo siku ya Jumapili, katika kiwanja
ambacho Wazungu walikuwa wakicheza gofu, ambako mwaka mmoja uliopita Gavana
Edward Francis Twining alitoa hotuba iliyowavunja moyo Waafrika, Nyerere alihutubia
mkutano wa hadhara. Kamwe haijapata kutokea kabla ya siku ile katika historia
nzima ya Jimbo la Kusini, watu wengi kiasi hicho kujumuika mahali pamoja.
Wazungu na Wahindi pamoja na askari, watu wakiwa wamekaa na wengine wamesimama
katika ya jua kali walikuja kumsikiliza Nyerere akihutubia. Ili kuhakikisha
amani na usalama pale mkutanoni serikali iliweka askari waliouzunguka uwanja
mzima wa mkutano. Nyerere aliwafikishia watu ule ujumbe wa TANU wa kuwa,
kutawaliwa ni fedheha, na Waafrika wa Tanganyika lazima wadai uhuru wao.
Uingereza ilikuwa ikiitawala Tanganyika chini ya udhamini kwa niaba ya Umoja wa
Mataifa, na wakati ukiwa muafaka inabidi Uingereza ikabidhi nchi kwa wananchi
wenyewe. TANU ilikuwa imewasili Jimbo la Kusini.
Wasomaji
wapenzi katika makala yangu iliyopita nilimpa changamoto Mzee Halimoja aeleze
ni akina nani waliingiza TANU kwao huko Masasi na Peramiho. Ukweli ni kuwa hata
kugusia hili katika makala yake iliyopita hakuthubutu. Nimempa changamoto
aeleze hicho anachokiita “mchango wa pekee wa Nyerere” katika kupigania uhuru
wa Tanganyika. Hilo vilevile limemshinda. Nashukuru kuwa kanijibu ingawa
kakwepa baadhi ya mambo muhimu lakini kwa kufanya hivyo kanipa mimi nafasi ya
kueleza yale ambayo naamini wengi walikuwa hawayajui. Nyerere hakuwa peke yake
katika kuupigania uhuru wa Tanganyika wala hakuandika katiba ya TANU wala
harakati za kupigania uhuru hakuzianzisha yeye. Nadhani haya niliyoandika
yanatosha kwa sasa na ningependa kumaliza kwa kuuliza swali. Nani leo
anawakumbuka wazalendo hawa nilowataja katika makala haya? Je hawastahili watu
hawa kuenziwa pamoja na Nyerere?
0 comments:
Post a Comment